Monday, May 24, 2010

Je huu ndio wajibu wa ndoa!

`Mimi najuta kuolewa, nashangaa nyie mnaolalamika kuwa hampati waume wa kuwaoa, mngelijua kasheshe, suluba, bugudha na utumwa uliopo humo ndani mwa kitu ndoa, mngelifikiria sana hili swala la ndoa, na ni bora ukawa na uhakika na huyo unayemtaka. Lakini hata hivyo, mbona mimi nilikuwa na uhakika huo, lakini siku nilipotumbukiza mguu wangu ndani ya nyumba ya ndoa, nilitamani mlango ufunguke nitoke nje, lakini ilikuwa nimeshachelewa…’ Hii ilikuwa hotuba ya mama mmoja kwa wenzake waliokuja kumtembelea.


`Hapana, usemayo unaangalia upande wako tu, hebu tueleze ni masibu gani yaliyokukuta, ili nasi tujihami nayo?’

‘Siku nilipofika nyumbani kwa mume wangu, nilikaribishwa na mawifi na shemeji zangu kwa sangwe, kwenye jumba kama la kathiri, humo wanaishi familia yote. Mwezi ule wa kwanza, nilijiona kama malkia ndani ya nyumba ya mfalme. Kila kitu kilikuwepo, lakini wao hawakutaka kuweka mfanyakazi wa nyumbani, waliniambia kuwa kwasababu wao wapo hakuna haja ya kumuajiri mtu, nikakubaliana nao, kwani hata nilipotoka hatukuwahi kuajiri mfanyakazi wa ndani, huwa tunajituma wenyewe!

Mara mume akaondoka ki-kazi, yeye hufanya kazi za masafwa marefu, kwahiyo akiondoka, hukata mwezi, akirudi hukaa siku mbili au tatu, na huondoka tena. Alipoondoka, nilishangaa, watu wote wakawa wananituma mimi kazi, mara wifi tuna njaa, mara shemeji leo utatupikia nini, waume zako tuna njaa. Mimi kwasababu nimezoea kazi, nikawa nafanya watakavyo.

‘Kila akiondoka, mimi hugeuka mtumwa, nafanya kazi zote za ndani, kuhudumia familia, kuwalisha shemeji zangu na mawifi, wao hulala, hujikalia au kutembea. Cha ajabu ndugu yao akirudi wanakuwa tofauti, hufanya kazi zote na mimi hawaniruhusu kugusa kitu, na kumwambia ndugu yao kuwa wao hawataki kumtesa wifi au shemeji yao. Hiki ndichi kilichoniuma, kwanini hawasemi ukweli, nisingechoka mapema hivyo, ila unafiki wao ndio ulioniuma sana….’

‘Niliamua kumweleza ndugu yao kinamna, nikiogopa kuigombanisha familia, na ndugu yao ambaye ni mume wangu alishangaa na kusema, mbona nikiwepo sijaona wakikuruhusu kufanya kazi, mbona nashindwa kuelewa kwasababu wao wenyewe wananiambia, wewe hawakuruhusu kabisa kufanya kazi, wanakuhudumia, kukufulia , kukupikia nk…’ kaka mtu hakuamini.

`Kama huamini basi, ila ukweli ndio huo ninaokueleza, ndugu zako ni wanafiki, hugeuka kama kinyonga. Nisingekueleza haya kama wangesema ukweli, lakini yote ni heri ipo siku utajionea mwenyewe’ nikajitetea.

‘Siku anaondoka kesho aliwaita kikao nakuwasema, na wao walijitia kushangaa, na kusema hilo halipo na halitatokea. Akaondoka, baadaye wanafamilia waliniita bila kaka yao kuwepo na kuniuliza, kuwa kuna tatizo gani, kwani wao wamefanya kipii kigeni, wakasema, kaka yao akiwepo inabidi wafanye kila kitu ili wanipe muda wa kukaa mimi na mume wangu, lakini akiondoka, inabidi na mimi nisaidie kazi za nyumbani…wakasema, kama naona kazi ni nyingi , nifanye ninazoweza. Wakaongezea, wao wanafikiri kufanya hivyo ndio wajibu wake, ndio wajibu wako katika ndoa. Wakamalizia kwa kuniomba samahani, halafu wakatawanyika na tabia ikawa ile ile!

‘Huo ndio wajibu wa ndoa nyie mnaotaka kuolewa’ akamalizia Yule mama.

Haya ni baadhi ya madhila katika ndoa, na wengi wakiyapata hukimbilia kuilaumu ndoa, lakini tujiulize kiuweli haya ndio masharti ya ndoa, na je yakitokea ndio sababu ya kuihujumu ndoa kuwa haifai? Hapana, hayo ni mawazo ya ubinafsi na tusiyachukulie kama msingi wa ndoa. Ndoa ni sehemu inayokamilsha ubinadamu, kuwa mwili mmoja, na kila mmoja ajihisi nafasi sawa na mwingine. Jamabo la muhimu ni kushirikiana, kuambizana na kuvumiliana.

Na kwa hili lilomkuta huyu mama nafikiri ni vyema angemmshauri kaka yake afanya uchunguzi na pindi akigundua kama kweli ana hekima na upendo atalisuluhisha na huo wajibu wa ndoa utawekwa sawasawa. Kuna haja ya kuelezana hili kiundani siku tukipata nafasi.